RAIS mstaafu Benjamin Mkapa ametuma salamu za rambirambi kutokana na
kifo cha mchumi mkubwa Tanzania na mzalendo Tanzania Sir Jayanti
Chandelier( 89) ‘Andy Chande’ aliyefariki Alhamisi asubuhi mjini
Nairobi, Kenya.
Taarifa kwa vyombo vya habari ilisema Mkapa amepokea taarifa ya kifo cha
Chande kwa masikitiko makubwa. “ Nimepokea kwa masikitiko makubwa kifo
cha Sir J K Chandelier. Alikuwa raia muaminifu kwa Tanzania aliyechangia
uelewa na ujuzi wake wa biashara kwa uchumi wa nchi,” alisema.
Alisema Chande alitumia muda mwingi kufanya shughuli za kijamii ambapo
mchango wake katika kuhudumia shule ya viziwi Buguruni utabakia kuwa
alama ya kihistoria. Alisema waliofanya kazi naye katika bodi za kampuni
mbalimbali za binafsi na umma watamkumbuka kwa uwezo wake wa kuchambua
matatizo na kutoa mapendekezo ya kuyakabili.
“Nimemfahamu kwa miongo minne tangu nilipokuwa Mhariri wa Magazeti ya
TANU na serikali, wakati wa urais wangu na baada ya kustaafu kwenye
shughuli za umma. Wakati wote alishauri bila chuki, hofu wala
upendeleo,” alisema.
Aliongeza kuwa Chande atabakia kuwa mzalendo, atakayekumbukwa na familia
na marafiki na urithi wake utabakia kwenye historia ya nchi. Maziko ya
Chande aliyefariki baada ya kuumwa tumbo kwa muda mfupi kutokana na
maambukizi, yatafaika Jumanne asubuhi katika makaburi ya Hindu, Dar es
Salaam.
Msemaji wa familia, Joseph Mapunda alisema heshima za mwisho zitatolewa
nyumbani kwake Barabara ya Msasani Namba 366a kuanzia saa 2:30 asubuhi.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni